Waathirika mabomu ya Mbagala waishinda Serikali mahakamani
Bomu likiwa limeharibu moja ya nyumba iliyopo katika eneo la
Mbagala jijini Dar es Salaam. Picha na Maktaba
KWA UFUPI
Waathirika hao ambao nyumba zao ziliharibiwa kwa mabomu,
wamefungua kesi Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, dhidi ya Katibu Mkuu wa
Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa na Mwanasheria Mkuu wa Serikali.
Dar es Salaam.
Waathirika wa mabomu yaliyolipuka Mbagala na kusababisha vifo na
uharibifu mkubwa wa mali za wananchi, wameibwaga Serikali mahakamani baada ya
kushinda pingamizi la Serikali dhidi ya kesi yao.
Waathirika hao ambao nyumba zao ziliharibiwa kwa mabomu,
wamefungua kesi Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, dhidi ya Katibu Mkuu wa
Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa na Mwanasheria Mkuu wa Serikali.
Katika kesi hiyo ya madai namba 181 ya mwaka 2011, wadai,
Aulerian Temba, Athuman Mtauka, Elovan Agustino na Catherine Isaya kwa niaba ya
wenzao 76, wanapinga malipo ya fidia yaliyotolewa na Serikali baada ya nyumba
zao kubomolewa kwa mabomu hayo.
Wanadai kuwa malipo hayo ni madogo mno kulinganisha na uharibifu
uliotokea, hivyo wanaiomba Mahakama pamoja na mambo mengine iwaamuru wadaiwa
(Jamhuri) iwalipe fidia kwa mujibu wa uthamini walioufanya kwa kumtumia
mthamini binafsi.
Serikali iliweka pingamizi katika shauri hilo ikiiomba Mahakama
hiyo iitupilie mbali kesi hiyo kwa kuwa imefunguliwa nje ya muda wa ukomo wa
kufungua kesi ya madai.
Hata hivyo, jana Mahakama Kuu katika uamuzi wake ilikubaliana na
hoja za wadai kupitia kwa Wakili wao Edson Mkisi kuwa kesi hiyo imefunguliwa
ndani ya wakati na kwamba Jamhuri haikuainisha sheria yoyote inayounga mkono
pingamizi lake na hivyo kulitupa.
Akitoa uamuzi huo, Jaji Dk. Fauz Twaib anayeisikiliza kesi hiyo
alisema pingamizi hilo la Jamhuri halina msingi wowote kisheria. Hivyo aliamuru
shauri hilo liendelee katika hatua ya kupanga namna ya kuliendesha katika hatua
ya usuluhishi, Mei 28, mwaka huu.
Awali, Jamhuri iliwasilisha pingamizi hilo mahakamani hapo,
ikidai kuwa tayari wadai hao walishalipwa fidia yao, lakini mahakama
ilipoiamuru iwasilishe mahakamani hapo vielelezo vya malipo hayo, ilishindwa
kufanya hivyo kabla ya baadaye kurudi tena na pingamizi hilo ambalo
lilitupiliwa mbali jana.
Wadai hao wanadai kuwa malipo ya fidia waliyopewa yalikuwa
hayatoshi hata kununua mfuko mmoja wa saruji na wengine walilipwa fedha ya
kununulia mkate tu.
Wanadai kuwa kwa nyumba zenye thamani ya zaidi ya Sh50 milioni,
kuna waliolipwa fidia ya Sh12,000 na wengine Sh1,200 tu.
Mabomu hayo yalilipuka Aprili 29, 2009 katika Kambi ya Jeshi la
Wananchi (JWTZ) KJ 671 na kusababisha vifo vya watu zaidi ya 25, huku mamia ya
watu wakijeruhiwa na familia nyingi kukosa makazi baada ya nyumba zao kubomoka
kabisa
.
.
No comments: